Uchimbaji dhahabu Buzwagi kukoma Machi 2021

Uchimbaji wa dhahabu katika mgodi wa Buzwagi, ulioko Kahama, Shinyanga nchini Tanzania unatarajiwa kufungwa Machi, 2021.

Taarifa zilizotufikia zinaeleza kuwa kufungwa kwa mgodi huo kunafuatia kukosekana kwa kiwango cha dhahabu iliyotatajiwa.

Imeelezwa kuwa kiwango kijachopatikana sasa ni kidogo mno kiasi cha kushindwa hata kupata mapato ya uendeshaji wa shughuli za uchimbaji na mahitaji mengine.

Wafanyakazi kupunguzwa

Aidha, tumedokezwa zaidi kuwa tayari taratibu za kupunguza wafanyakazi zimeanza, huku wengi waliokuwa na mikataba ya muda mrefu wakitakiwa kujadiliana na uongozi ili kuachana “salama.”

Taarifa zinaeleza kuwa kufungwa kwa mgodi huo, mwaka mmoja kabla ya muda uliokuwa umewekwa na wamiliki wake, Kampuni ya Barrick Gold, kumesababishwa pia na kushuka kwa bei ya dhahabu katika soko la dunia.

Inasemekana kwamba ratiba ya awali ilielekeza mgodi kufungwa mwaka 2020, lakini kulikuwepo na mgogoro na serikali juu ya mkakati wa ufungaji wa mgodi (mine closure plan) ambayo haikuwa inaridhisha kwa serikali kuikalia kooni Barrick, baada ya Serikali pia kuja na ‘mining closure plan’ yake (MCP) mwaka jana ambayo ina maelezo mengi ambayo ni kama inawabana watu wa migodi waweze kudai tena eneo lililochimbwa angalau liwe kwenye hali nzuri ambapo panaweza kufanyika shughuli za kibinadamu…

Kuwepo kwa shughuli za uchimbaji wa dhahabu Buzwaji kuliongeza mzunguko wa fedha katika eneo hilo na jirani, hivyo kukuza uchumi wa halmashauri, wananchi na ongezeko la kodi kwa nchi.

Barrick hawajakata tamaa

Hata hivyo, taarifa zaidi zinaeleza Barrick wanapanga kukutana na Serikali ya Tanzania ili kuomba vibali vya kuanza utafiti na uchambuzi wa kuwepo kiwango kikubwa cha dhahabu katika maeneo jirani na Buzwagi. 

Ikiwa watakubaliana, huenda shughuli za kusaka dhahabu ikahuisha tena uchumi na  maisha ya watu wa Buzwagi na maeneo jirani.