Maalim Seif kuwekwa chini ya uangalizi maalum

Vyombo vya usalama Zanzibar, usiku huu vimepanga kumzuia Maalim Seif Shariff Hamad asitoke nyumbani kwake, Chukwani, Zanzibar.

Maalim Seif, ambaye ni mgombea urais visiwani humo kupitia ACT – Wazalendo, katika mkutano wake wa mwisho wa kampeni kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja, Zanzibar aliwaamuru wanachama na wafuasi wake kwenda kupiga kura kesho, Oktoba 27, siku ambayo ni maalum kwa baadhi ya watendaji wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) na vikosi maalum vya usalama.

Maalim na chama chake waaamini kuwa ZEC, Chama Cha Mapinduzi (CCM) watatumia mwanya huo kuiba kura za urais na kumuongezea Dk. Hussein Mwinyi, mgombea urais wa chama tawala.

Tayari ZEC imekanusha tuhuma hizo na kuziita “uzushi” wa viongozi wa ACT-Wazalendo.

Taarifa za uhakika zilizotufikia zinaeleza kuwa kwa kuwa hatua ya Maalim Seif kwenda kituoni ili kupiga kura kesho, inaweza kuleta vurugu kubwa miongoni mwa wafuasi wake na vyombo vya usalama.

Jana Maalim Seif aliapa kwamba yuko tayari kufa ikiwa kufanya hivyo itakuwa ni njia ya “kuwakomboa” Wazanzibar kutoka kwenye makucha ya mkoloni, aliyemtaja kuwa ni “Tanganyika.” Tanganyika ni ni jina la Tanzania kabla haijaungana na Zanzibar mwaka 1964.

Imebainika kuwa Jeshi la Polisi, kupitia kikosi chake cha FFU, Jeshi la Wananchi na baadhi ya maofisa wa Idara ya Usalma wanahusika katika zoezi la kumdhibiti Maalim Seif na wafuasi wake kusogelea vituo vya kupigia kura, ambavyo taarifa zinaeleza kuwa vingi viko ndani ya kambi za Jeshi.