Kumekucha: Chenge, Adadi, Ngeleja waiandikia CCM kutaka sababu za kuenguliwa

Makada watatu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao majina yao hayakupitishwa kugombea ubunge, wamewasilisha barua kuomba sababu za kukatwa.

Wawili kati ya hao watatu, licha ya kuongoza katika kura za maoni, majina yao yalikatwa na Halmashauri Kuu ya chama hicho (NEC), hivyo kuenguliwa kupeperusha bendera ya chama hicho tawala kwenye uchaguzi mkuu unaofanyika Oktoba 28 l, mwaka huu, 2020.

Taarifa zilizotufikia kutoka Makao Makuu ya CCM jijini Dodoma na kwa watu walio karibu nao zinaeleza kuwa wabunge hao wa Bunge lililomaliza muda wake, wanataka kupewa maelezo ya sababu za kuenguliwa kwao ili ikiwezekana watambue endapo zinahusiana na jinai.

Kwamba endapo zitahusishwa na jinai, hasa rushwa; wapate muda wa kueleza kilichotokea wakati wa mchakato wa kura za maoni.

Wanaotajwa kuwasilisha barua hizo ni Andrew Chenge, aliyekuwa mbunge wa Bariadi na Adadi Rajabu, aliyekuwa Muheza. Mwingine ni Willliam Ngeleja wa Sengerema.

Chenge na Adadi waliongoza kura za maoni katika maeneo hao, huku Ngeleja akamata nagasi ya pili katika kusaka kura za wajumbe.

Makada wote ni watumishi waandamizi wa Serikali zilizopita. Chenge amewahi kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ngeleja akiwa Waziri kwa kipindi na Wizara tofauti, huku Adadi akiwa Balozi na Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI).

Inaelezwa kuwa makada hawa wana hofu ya majina yao kuchafuliwa endapo sababu za kuenguliwa kwao ni rushwa.

Inaelezwa kuwa CCM, imekuwa ikitangaza kwamba itawaengua watia nia wa ubunge ambao watabainika kujihusisha na rushwa katika kusaka kura za wajumbe.