Kubenea aburuzwa mahakamani na aliyekuwa mfanyakazi wake

Saed Kubenea, aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Ubungo, Dar es Salaam kupitia CHADEMA, ameburuzwa mahakamani kwa tuhuma za kushindwa kulipa Sh milioni 9.

Kubenea aliyehamia chama cha ACT-Wazalendo, anatakiwa kufika Mahakama ya Mwanzo Kawe jijini Dar es Salaam, Agosti 17, 2020 ambako shauri hilo limefunguliwa.

Anayemdai ni Deusdedith Kahangwa ambaye aliyekuwa mwandishi katika gazeti la Kubenea, kupitia Kampuni ya Hali Halisi Publishers.

​Kahangwa anadai fedha hizo baada ya Kubenea kushindwa kulipa stahiki zake kwa mujibu wa mkataba waliokubaliana wakati wa kuanza kazi.

​Uchunguzi wetu umebaini kwamba, Mahakama hiyo, Juni, mwaka huu ilimpa ushindi Deusdedith hivyo Kubenea kuamriwa kulipa kiasi hicho cha fedha.

​Hata hivyo, tangu kutolewa kwa hukumu hiyo Kubenea amekuwa ‘akikimbia’ kutekeleza hukumu ya mahakama.

Kutokana na hali hiyo, Deusdedith ameiomba Mahakama imlazimishe Kubenea kulipa fedha hizo.

Taarifa zilizotufikia wakati muda mfupi kabla ya kuchapa habari hii, zinaeleza kwamba Kubenea alikuwa akijiandaa kukata rufaa kupinga hukumu hiyo ya kulipa Sh. milioni 9.